Friday, 21 August 2015

Nilishtuka baada ya kuona nyuso za wasichana wanaouza miili yao, wengi ni chini ya miaka 18

Ilikuwa kama muda wa saa mbili usiku nilipokatiza maeneo yao wanapojibanza ukutani wakisaka tonge na vijisenti kwa mahitaji mengine muhimu.

Nilipotokeza kwenye uchochoro ambapo huwa wanajipanga kusubiria wateja walianza kunivamia huku kila mmoja akijinadi kuwa mzuri zaidi ya mwenzie.

Nikiwa nimeshikwa na kigugumizi kilichofungamana na uwoga nilikosa cha kusema huku nikiwa nakodolea macho kwenye nyuso zao.

Kunipotezea ndilo jambo lililofuatia baada ya kugundua kuwa sikua mteja wao. Walinipotezea huku wakiambiana kuwa achana nae huyo hana lolote.

Kitendo cha kupotezewa kukawa ndio kupona kwangu. Daaa! Nikaendelea na safari yangu kuelekea barabarani huku kijasho chembamba kikinitoka.

Niligeuza shingo na kutazama nilikotoka. Macho yangu yakakutana na bango lililoandikwa Kimboka bar, nikajiwa na kumbukumbu kwamba nilishawahi kuambiwa kuwa eneo hilo lina wanawake wanaouza miili.

Kumbe ndio hapa! Nilijiambia mwenyewe. Lakini kilichoniumiza ni nyuso za akina dada nilizozikodolea. Nyuso zilizojaa mengi ya kuzungumzia. Nyuso ambazo zinajieleza kwa kuziangalia tu.

Nyuso zao tu zilikuwa kipimo tosha cha kupima umri wao. Maskini, ni wasichana wadogo ambao kwa kuangalia nyuso zao ni wa juzi tu.

Yaani wengi wao ni chini ya umri wa miaka 18, umri ambao bado ni wa mtoto wa shule aliyetakiwa kuwa nyumbani mezani akijisomea alichofundishwa na mwalimu wake.

Ni hatari sana kwa maisha yao na kizazi kijacho. Siwezi kujua sababu iliyowafanya wajiingize kwenye biashara hile lakini haijalishi nini kimewatumbukiza, ni hatari sana kwao na kwa taifa kwa kuwa nguvu kazi inaangamia.

Image result for malaya wa buguruni