Mchakato wa usaili kwa ajili ya kujaza nafasi za Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji zinazohitajika, unaendelea licha ya waombaji 4,834 kuchujwa katika awamu ya kwanza. Kati ya waombaji 6,116 waliofanyiwa usaili hivi karibuni jijini Dar es Salaam, waombaji 1,281 ndiyo wamebaki wakisubiri duru ya mwisho ya usaili, wabaki 70 watakaojaza nafasi hizo.
Taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Isaac Nantanga, ilisema awali waombaji 10,801 waliitwa kwa ajili ya usaili wa kwanza baada kupokea maombi yao ingawa waliohudhuria walikuwa 6,115.
Alisema hatua hiyo iliwezesha kupatikana kwa kundi litakalofanyiwa usaili mwingine Juni 23 hadi Julai 3, mwaka huu.
Kwa mujibu wa Msemaji huyo wa Wizara, katika awamu ya pili, usaili utakuwa wa maswali ya ana kwa ana ukilenga kupima uwezo wa msailiwa kujieleza na kufafanua mambo.
Alisema usaili wa kwanza, ulikuwa wa kuandika na ulihusisha maswali ya hesabu na ufahamu wa jumla.
Kuchaguliwa kwa wasailiwa hawa kulifanyika baada ya kusahihisha majibu yao na majina kuingizwa katika mfumo wa kimtandao ambao ulisaidia kuchagua wasailiwa waliopata alama 50 na kuendelea.
Taarifa ya Wizara imeweka majina ya wasailiwa katika tovuti yake; www.moha.go.tz na ya Idara ya Uhamiaji, www.uhamiaji.go.tz.
Wasailiwa wote wanatakiwa kwenda na vyeti vyao halisi vya kuzaliwa, vya shule na picha mbili za pasipoti.
Usaili wa awamu ya kwanza uliofanyika Dar es Salaam hivi karibuni, uligeuka gumzo kutokana na idadi kubwa ya watu walioitwa, jambo ambalo halijawahi kushuhudiwa.