Wednesday, 9 April 2014

'Sisi kwa Sisi', shirika lililofungiwa kwa kuhamasisha ushoga nchini.

Serikali ya Tanzania imefuta usajili wa shirika moja lisilokuwa la kiserikali kwa sababu ya kuhamasisha mapenzi ya jinsia moja katika jamii.

Shirika hilo kwa jina Sisi Kwa Sisi lilisajiliwa baada ya kudai kuwa malengo yake yalikuwa ni kusaidia jamii.

Tanzania imesema imechukua hatua ya kufutilia mbali usajili wa shirika hilo kwa kukiuka sheria
za nchi na kwenda kinyume na malengo ya usajili wake.

Mkurugenzi wa usajili wa mashirika yasiyo ya Kiserikali nchini Tanzania, Maseli Katemba,
amesema kuwa shirika hilo la Sisi kwa Sisi limekiuka malengo yake ya awali ya kuwapa elimu na misaada ya kifedha wananchi lakini
mambo yakawa tofauti.

"Baada ya kufuatilia tumegundua kuwa sasa wanatilia mkazo kuwasaidia watu wa jinsia moja,"
alisema Bwana Katemba.

Bwana Katemba amesema kuwa Serikali itaendelea na kuyasaka makundi mengine kama
hayo ambayo yanaendesha maswala yaliyo kinyume na sheria za Tanzania.